Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, Ayatullah Alireza A’rafi, Mkurugenzi wa Hawza nchini Iran, baada ya darsa ya juu ya fiqhi na usul, huku akisisitiza umuhimu wa kuwepo wanafunzi wa dini katika uwanja wa tablighi, alielezea hali ya dini duniani leo kuwa ni hali ya kipekee yenye fursa pamoja na hatari kubwa, na akasema: “Leo dini, zaidi ya wakati mwingine wowote, inahitaji wanazuoni wenye fikra na wapiganaji; jambo lilelile lililosisitizwa katika ujumbe wa hivi karibuni wa Kiongozi Mkuu wa Mapinduzi. Sasa walimu wote, watafiti na wanafunzi wa dini, kwa kuhamasika na maraji' wakuu na wakubwa wa hawza, wanapaswa kujiunga na wimbi kubwa la walinganiaji wa dini, msafara wa ‘Balagh Mubin’ na mkondo wa kuhama na kutumwa.”
Akiashiria kuwa, kwa upande fulani ana matumaini kuhusu hali mpya, alisema: Katika vipindi fulani, kuingia hawza hakukuambatana na hatari kubwa au angalau hatari hizo hazikutambuliwa ipasavyo. Lakini leo, pamoja na fursa kubwa, kuna hatari kubwa pia. Hatari hizi, kwa upande mmoja, ni zenye baraka; kwa sababu wale wanaokuja kuzielekea dini na hawza leo husimama imara kwa ajili ya dini na hawza na hupata thamani kubwa zaidi.
Mkurugenzi wa Hawza, huku akirejea mfano wa kutoa matumaini wa Ashura, alisisitiza: Hakujawahi kuwepo tukio la kukatisha tamaa zaidi kwa upande wa haki kuliko alasiri ya Ashura, lakini msafara ule uliobaki kwa matumaini yake ulibadilisha historia. Leo pia tunapaswa kuchukua matumaini kutoka Ashura na kwa roho hiyo hiyo kuendelea katika njia ya kuitumikia dini, watu wema na vijana wapendwa.
Ayatullah A’rafi aliitaja tablighi kuwa ni jukumu kuu la hawza na akasema:Leo tablighi katika mifumo yote ya zamani na mipya — hata zaidi ya msikiti na mimbar rasmi — ni jukumu la lazima. Ni lazima kuwasiliana na makundi mbalimbali na kizazi cha vijana. Kwa kuzingatia likizo ya takribani miezi miwili inayokuja, imesisitizwa kwamba kambi na programu maalum za likizo zihamishiwe majira ya kiangazi au nyakati nyingine, ili fursa ya tablighi isichukuliwe kutoka kwa wanafunzi na walimu.
Aliongeza kuwa: Pia kuna mashauriano yanayoendelea ili uendeshaji wa baadhi ya masomo usipanuliwe katika kipindi cha likizo na mwezi mtukufu wa Ramadhani, kwa sababu kipaumbele cha sasa ni uwepo wa wanafunzi wa dini katika uwanja wa tablighi na Balagh Mubin.
Mkurugenzi wa Hawza akisisitiza jukumu la kuwasiliana na kizazi kipya, alisema: Mawasiliano ya kielimu na ya huruma kati ya wanazuoni na jamii, hasa wanafunzi wa shule, wanafunzi wa vyuo, walimu na vijana kwa ujumla, ni dhamira muhimu sana. Wakati mwingine hata kusikiliza tu changamoto za hadhira kunaweza kujenga uhusiano na uaminifu wa kina, na hili lenyewe ni aina ya tablighi yenye athari.
Mtaji wa kijamii wa ulamaa, heshima ya nchi, kusimama dhidi ya maadui, na ushirikiano na wanataaluma na wasomi katika kuimarisha mshikamano wa wananchi, ni mahitaji ya leo ya nchi, na tablighi inapaswa kufungua njia hii.
Ayatullah A’rafi alisisitiza: Dhamira hii leo ipo zaidi kuliko wakati mwingine wowote na inahitajia watu wenye fikra na wapiganaji. Pamoja na hatari na mipaka iliyopo — ambayo baadhi yake iko nje ya uwezo wa hawza — ni lazima njia ipatikane na kuendelea kwa nguvu. Hakuna anayepaswa kujidanganya kwa visingizio mbalimbali na kubaki nyuma ya tablighi, ufafanuzi wa haki na Balagh Mubin.
Mkurugenzi wa Hawza mwishoni aliongezea: Maulamaa wanapaswa kujiona wako pamoja na wananchi, wanawahurumia, wanadai mahitaji yao, wanawaongoza kuelekea maadili na dini, na kuwa watumishi wao.
Maoni yako